Moses Wetangula aukosoa mswada wa Punguza Mzigo.

Mswada wa Punguza Mizigo wa Chama cha Thirdway Alliance ulioidhinishwa na Tume ya Uchaguzi, IEBC unaendelea kuibua hisia mbalimbali miongoni mwa viongozi nchini.

Seneta wa Bungoma, Moses Wetangula ambaye pia ni Kinara wa Ford Kenya ameukosoa mswada huo akisema hatua ya kutaka kupunguza idadi ya uwakilishi wa mwananchi bungeni kwa madai ya kupunguza gharama ya kuendesha serikali kamwe haitamsaidia mwananchi kwani ni kuondoa huduma mashinani.

Akizungumza mjini Nakuru, Wetangula amesema hatua hiyo haiwezi kusuluhisha changamoto zinazowakumba wananchi badala yake itaathiri kasi ya maendeleo.

Wetangula aidha amesema hatua ya kupendekeza kuondolewa kwa Bunge la Seneti kamwe haitasaidia kuimarisha huduma mashinani, kwani bunge hilo hupokea takriban shilingi bilioni 40 pekee kila mwaka ikilinganishwa na taifa la bajeti ya shilingi trilioni tatu.

Kauli ya Wetangula inajiri huku Mwenyekiti wa Baraza la Wahubiri na Maimamu wa Dini ya Kiislamu CIPK katika eneo la Bonde la Ufa Abubakar Bin akiwataka viongozi wa dini nchini kuunga mkono mswada huo na hata kuhamasisha umma kuupigia kura iwapo kutaandaliwa kura ya maoni.

Kulingana naye, Bunge la Seneti na lile la kitaifa yanatekeleza jukumu moja na hivyo kuondolewa kwa bunge la Seneti hakutaathiri huduma mashinani.

RELATED POSTS

[products limit=”4″ columns=”4″ orderby=”date” order=”DESC” ids=”1381,1387,1376,1369″]
Exit mobile version